
1985 - 2007
64. Kanisa La Mavuno
Je, limejiandaa kwa mavuno ya siku za mwisho?
Support Pages
Index to All Lessons School of Finances
World Christian News
Who
Are We? Site Index
Katika Biblia Yako Soma
Matendo 4
Mstari wa Kukariri
Basi sasa, Bwana yaangalie matisho
yao; ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote, ukinyosha mkono
wako kuponya; ishara na maajabu vifanyike kwa jina la Mtumishi wako mtakatifu
Yesu (Mdo 4:29,30).
Baadaye Zungumzieni Jambo Hili
Hebu fikiria kwamba watu kwa
maelfu ghafla wamekuja kwenye makanisa yenu, au kwamba mateso yameanza. Ni nini
kingetokea kwenye makanisa hayo?
Jambo La Kufanya Kabla Hatujakutana
Tena
Hebu fikiria kwamba waamini wapya
1,000 wameamua kumfuata Yesu, na jengo lenu la kanisa lina uwezo wa kuchukua
watu 200 tu, na mchungaji wenu anawajali wote. Piga mahesabu upate gharama za
kuajiri wachungaji wengine zaidi na ama kupanua jengo la kanisa au kujenga
majengo mengine maeneo mengine ya wilaya.
Kazi Ya Kuandika Ya Stashahada
Andika taarifa ya kurasa mbili
ukilinganisha miundo ya madhehebu ya siku hizi na wepesi wa kiutekelezaji wa
muundo wa Agano Jipya. Eleza kwanini mojawapo ni bora kuliko mwingine.
Tafakari Andiko Hili Neno Kwa Neno
Mdo 2:46,47
Tumia Dakika Moja Kuubadilisha Ulimwengu
Ombea taifa la Burkina Faso. Idadi ya watu ni 8,000,000 waliogawanyika katika makundi makuu manne: Waislamu, waislamu jina, maskini, na Wakristo wanaotuma wamishenari katika nchi za Afrika Magharibi.
Chagua hapa > 64chart ili uone mchoro kwa ajili ya somo hili
Katika karne ya kwanza divai mpya iliyomiminwa na Roho wa Mungu ilihitaji viriba vipya vya kuihifadhi na kuiivisha. Watu kwa maelfu ghafla waliamua kumfuata Yesu lakini tatizo halikuwa mbali!
Ingekuwaje Kama Hilo Lingetokea Leo?
Katika ulimwengu mzima kuna mielekeo miwili ya waziwazi inayoonekana ndani ya kanisa la leo. Je, utafanyaje ikiwa moja kati ya haya litakuja kwenye taifa lako?
Ukuaji Mkubwa
Kule nchini Argentina, Korea Kusini na maeneo kadhaa ya Afrika mamilioni ya watu wameamua kumfuata Yesu na wanakuja kanisani.
Mateso Makali
Katika miaka ya karibuni makanisa mengi yamechomwa moto katika nchi za Bosnia, Uingereza, India, Indonesia, Ireland, Liberia, Pakistan, Senegal, Sierra Leone na Sudan. Na nchini Rwanda wakati wa machafuko waamini walikimbilia makanisani, lakini maadui zao waliwafuatilia huko na kuwaua kwa maelfu.
Ni Unabii Au Ni Swali Tu?
Ikiwa ni katika kukua au mateso, au yote kwa pamoja, je, utamaduni wetu katika ujenzi wa majengo utakidhi, serikali ya kanisa na makasisi wenye elimu je?
Katika Kukua Wewe Utafanya Nini?
Unaweza kuwajaza hao watu wapya katika majengo yaliyopo sasa na kutazamia viongozi wa kulipwa kufanya kazi kwa juhudi mara kumi zaidi? Na iwapo utahitaji mara moja majengo zaidi, fedha zote hizo zitapatikana wapi?
Katika Mateso Wewe Utafanya Nini?
Nchini Rwanda kanisa lilikwama lakini kule Uchina, mwaka 1948, wakati makanisa yalipofungwa, wachungaji kuuawa au kufungwa gerezani na wamishenari wote kufukuzwa, kanisa halikufa. Kwanini lisife? Ni kwa sababu hilo kanisa lilikuwa na uwezo wa kubadilika na mazingira yaliyokuwepo, likabadilika sura na kufanana na lile la Agano Jipya kimuundo. Lilikua kwa shida kutoka waamini 8,000,000 hadi kufikia kwenye 80,000,000 mnamo mwaka 1988.
Muundo Wa Agano Jipya
Kanisa linalotazamia mavuno ya nyakati za mwisho litakuwa tayari, kwa vyo vyote vile, kwa kuhakikisha kwamba muundo wake ni ule utakaowawezesha kukua na kudumu. Kitabu cha Matendo ni kitabu cha Mungu cha muundo wa kanisa. Hebu tuangalie na kugundua mikakati mitatu muhimu.
Kanisa, Sio Makanisa
Migawanyiko pekee tunayoiona ni ya kijiografia na si ya kidhehebu. Katika Biblia hakuna migawanyiko ya Kikatoliki, ya Kibaptisti au ya Kipentekoste; hata mbinguni haipo! Tunachokiona hapa ni Kanisa. Mjini Yerusalemu, kule Antiokia, Efeso, na kadhalika. Katika ukuaji tunahitajiana, kwa sababu wakati Yesu alipompa Petro samaki wengi, Petro aliwaita wavuvi wenzake kuja kumsaidia (Lk 5:4-7). Katika nyakati za ugumu vikundi mbalimbali vya kanisa husaidiana (Mdo 11:27-30).
1. Makanisa Mama
Makanisa makuu katika kitabu cha Matendo na katika Nyaraka yanajulikana kama makanisa mama kwa sababu ya uzima mpya yanayotoa kwa mikoa yake. Kanisa la Thesalonike lilikuwa ni mfano mzuri kwetu sote,(1The 1:7). Lakini Yerusalemu, Antiokia, Efeso, Filipi na mengine yalikuwa ni zaidi ya makanisa ya maeneo. Zaidi ya makusanyiko tu yalikuwa na shughuli za Roho Mtakatifu, maombi, uinjilisti, unabii na mikutano ya mafundisho. Kulikuwa na wingi wa viongozi, na jamii iliyo hai na inayojali, hasa huko Yerusalemu (Mdo 2:42-47; 4:32-34). Walipata mateso, na kukabiliana na changamoto za kisheria.
Yalikuwa Pia Vituo Vya Kitume
Je, kituo cha kitume ni nini? Ni kanisa la mfano wa kuigwa, ambapo mitume na watu wengine wamekusanywa na Roho Mtakatifu. Neno ‘kitume’ hasa lina maana ya kimishenari, kwahiyo kanisa mama linakuwa ni mahali pa kuondokea, na kituo cha kupatia watu, fedha na vifaa vingine kwa ajili ya umisheni; mahali ambapo mikakati ya umisheni inabuniwa na timu za kitume na misaada inapelekwa kwa makanisa mengine na kwa mataifa. Ni mahali pa ushirika, uamsho, uwajibikaji na msaada kwa watu wanaotumwa na Mungu, na wala si ‘piramidi’ linaloamrishwa na mtume asiye wa kawaida.
Je, Kanisa Mama Huwa Na Mnara?
Hadi kufikia karne ya nne hapakuwa na kanisa lenye mnara, wala jengo lenyewe! Ukuaji wa kasi, wingi wa watu maskini na mateso ya kikatili kulimaanisha kwamba kanisa lilipaswa kustahimili katika mazingira hayo na liweze kusambaa bila gharama za majengo, liweze kudumu hata katika vitisho, na liwe na watu wengi iwezekanavyo kwa ajili ya huduma.
Muundo Wa Kanisa La Nyumbani
Waliwezaje kufanya yote hayo? Ni kwa kutumia muundo wa kanisa la nyumbani na kukutana majumbani chini ya mwavuli wa kitume. Walikutana tu wote pamoja mara kwa mara. Tazama somo kuhusu Kanisa la Nyumbani.
2. Makanisa Binti
Watu kama Filipo walitoka kwenye kanisa mama, wakahubiri injili, wakawakusanya waamini wapya, na kuacha nyuma yao kanisa binti likitunzwa na viongozi wa kanisa mama hadi likomae (Mdo 8:4-17). Kanisa binti linapaswa kuwa la kimishenari kuanzia siku ya kwanza ya kuwepo kwake, likitafuta kuanzisha kanisa binti mwenzake (Tazama Kanisa Mama).
3. Timu Za Kitume Za Kimishenari
Sehemu ya mwisho, ncha ya mshale ya muundo wa Agano Jipya ni timu ya kitume (Mdo 13:1-4). Hawa ni watu walioitwa na Mungu ili wawaendee mataifa. Wanaachishwa shughuli zote katika maeneo yao na kuachwa waende zao. Njiani wanajitegemea, wanajitawala na kujirudufu wenyewe kuwa:
Makanisa mapya kama yale ya Galatia, (Mdo 14:21-25).
Shule mpya za mafunzo kama kule Efeso, (Mdo 19:9,10).
Kazi mpya ya umisheni, (Tit 1:5) (1Tim 1:3).
Timu mpya za kitume kama zile zilizotoka kwenye makanisa mengi, (Mdo 20:4).
Kisha wanarudi nyumbani na kutoa taarifa na
kushiriki katika uongozi wa kanisa mpaka watakapoondoka tena. (Angalia Kanisa la
Kimishenari).
Kwa Kumalizia Omba Kwa Ajili Ya Watu Wa Ulimwengu Ambao Hawajafikiwa Na Injili, Ukiwataja Kwa Majina
| Somalia | ||
|
Jina la Watu |
Lugha Yao |
Idadi Yao |
|
Dabarre |
Dabarre |
20,000 |
|
Garre |
Garre |
50,000 |
|
Jiiddu |
Jiiddu |
20,000 |

1985 - 2007
With many thanks to Pastor Dastan
Mboera, Dar es Salaaam, Tanzania
and EAPTC Nairobi, Kenya
for this revision and translation from the original English.
mboeradsk @ yahoo.com
© Dr Les Norman The DCI Trust, UK
Permission is granted to provide
copies at cost price for study purposes
but not for sale or commercial
purposes. Freely you have received, so please freely give.
Support Pages
Index to All Lessons School of Finances
World Christian News
Who
Are We? Site Index
www.dci.org.uk